Bodi ya Nishati Vijijini (REB) imeeleza kuridhishwa kwake na kasi ya usambazaji wa nishati ya umeme katika vitongoji vya Kisiwa cha Jibondo, kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mafia, mkoani Pwani.
Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti wa REB, Mhe. Balozi na Meja Jenerali Mstaafu Jacob Kingu, tarehe 27 Agosti, 2026 alipoambatana na Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kisiwani humo kukagua maendeleo ya mradi huo mkubwa ambao tayari umegharimu kiasi cha shilingi bilioni 8.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Meja Jenerali Kingu amesema kuwa kwa mara ya kwanza katika historia, vitongoji vya Kisiwa cha Jibondo vinatarajia kupata huduma hiyo ya nishati hivi karibuni. Alifafanua kuwa kazi kubwa iliyobaki kwa sasa ni ya usafirishaji wa umeme kwa kutumia waya maalum wa chini ya maji (Submarine cable) kutoka kisiwa kidogo cha Juani kwenda Jibondo, kazi inayotarajiwa kuanza kesho, tarehe 29 Agosti 2026, na kukamilika baada ya siku tano.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy, amesema kuwa maandalizi yote ya miundombinu ikiwemo ujenzi wa njia za kusafirisha umeme ndani ya kisiwa hicho yamekamika kwa asilimia 90 na ameongeza kuwa mara baada ya nyaya hizo za chini ya maji kuunganishwa, wananchi wataanza kuunganishiwa huduma hiyo mara moja.
Mhandisi Saidy amebainisha kuwa mradi huo umefanikiwa kwa ushirikiano wa REA iliyochangia shilingi bilioni 6.8 na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) lililochangia shilingi bilioni 2.
Katika hatua nyingine, Mhandisi Saidy ametoa wito kwa wakazi wa Jibondo kujiandaa kiuchumi ili kuutumia umeme huo katika kuboresha maisha yao na kuendesha shughuli za kimaendeleo, hasa ikizingatiwa kuwa sehemu kubwa ya wakazi wa eneo hilo wamejiajiri kwenye sekta za uvuvi, usindikaji wa mazao ya bahari, na kilimo cha mwani.
Wilaya ya Mafia ina jumla ya vitongoji 136, ambapo vitongoji 111 tayari vimeshafikishiwa huduma ya umeme. Vitongoji vingine 19 vipo kwenye mpango wa utekelezaji kupitia Mradi wa HEP II (B), huku vitongoji 6 vilivyobaki vikiwa ni hivyo vya Kisiwa cha Jibondo vinavyosubiri kuwashwa kwa umeme huo hivi karibuni.
Naye mmoja wa wakazi wa kisiwa hicho, Mzee Abdalah Hassan, ameishukuru Serikali kwa uwekezaji huo mkubwa na kueleza kuwa umeme huo utakuwa mkombozi mkubwa kwao.
"Umeme unahitajika kila mahali. Shuleni utasaidia kuchapisha mitihani na kujifunza kwa njia ya kompyuta, lakini pia utatupa wepesi wa kuandaa chakula na kuleta mwanga majumbani. Tumefarijika sana, ni faraja kubwa isiyo na kifani," amesema Mzee Abdalah.
- MWISHO –