BODI YA WAKURUGENZI YA REA WAKUTANA NA WAKANDARASI, PAMOJA NA WATENGENEZAJI WA VIFAA VYA MRADI WA UMEME VIJIJINI
1. Bodi ya Wakala wa Nishati Vijijini leo tarehe 08 Juni 2019 imekutana wa Wakandarasi wa Mradi wa REA Awamu ya III Mzunguko wa I katika Ukumbi wa Hazina, Dodoma kujadili changamoto mbalimbali zinazoweza kuchelewesha utekelezaji wa Mradi. Pia Menejimenti ya REA ilishiriki mkutano huo. Mradi wa REA Awamu ya III Mzunguko wa I unagharimu Shilingi Trilioni 1.2, ukiwa ni mradi mkubwa kusini mwa jangwa la Sahara ambapo vijiji 3,559 vitaunganishwa na huduma ya nishati ya umeme nchi nzima.
2. Bodi ya Wakurugenzi ilitaka kujua mahusiano mazuri kati ya Wakandarasi wa Mradi huo pamoja na watengenezaji wa vifaa vya mradi kama vile nguzo, nyaya, transfoma, mita na vifaa vingine. Mahusiano mazuri kati ya Wakandarasi wa watengenezaji vifaa hivyo yanaleta tija katika kuharakisha utekelezaji wa mradi.
3. Wakandarasi walieleza baadhi ya changamoto kuhusu kuchelewa kupata vifaa wanavyoagiza kutoka kwa watengenezaji. Bodi ilielezwa na watengenezaji wa vifaa hivyo kuwa wanavyo vya kutosha na watarekebisha kasoro zozote zilizojitokeza ili kuwawezesha Wakandarasi kukamilisha utekelezaji wa Mradi kwa wakati.
4. Bodi, baada ya kuwasikiliza Wakandarasi pamoja na watengenezaji wa vifaa vya mradi, ilieleza kuwa changamoto zilizoelezwa ziko ndani ya uwezo wa kutatuliwa. Changamoto kubwa iliyoonekana ilikuwa ni uelewa wa baadhi ya taratibu ikiwemo bondi inayowekwa na Benki.
5. Mkutano ulisisitiza kuwa Mradi wa REA Awamu ya III Mzunguko wa I utakamilika ifikapo Desemba, 2019 na Wakandarasi atakayechelewesha Mradi kwa mujibu wa Mkataba hawatavumiliwa.
Mkurugenzi Mkuu
Wakala wa Nishati Vijijini (REA)
Jengo la LAPF, Ghorofa ya 7
P. O. Box 2153
Dodoma, Tanzania
E-Mail: info@rea.go.tz
Tel: +255 262323504, +255 262323506, +255 262323507