Wakala wa Nishati Vijijini (REA), umesema usambazaji wa umeme vijijini unaendelea kuwa kichocheo kikubwa cha ukuaji wa uchumi kwa kufungua fursa za uzalishaji, ajira na uwekezaji, huku ukiboresha maisha ya wananchi kupitia maendeleo ya sekta mbalimbali za kiuchumi.
Akizungumza katika Maonesho ya Nane Nane katika Viwanja vya Nzuguni jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA, Mha. Jones Olotu, amesema uwekezaji wa Serikali kupitia REA katika miradi ya kusambaza umeme; umewezesha sekta mbalimbali za uzalishaji kukua kwa kasi na kuongeza mchango wake katika maendeleo ya uchumi wa vijijini.
“Lengo la REA si kusambaza umeme pekee yake bali kuhakikisha umeme unakuwa chachu ya kuleta maendeleo kwa kuwezesha viwanda vidogo na vya kati, biashara, huduma za kijamii pamoja na shughuli nyingine za uzalishaji vijijini,” amesema Mha. Olotu.
Ameeleza kuwa upatikanaji wa umeme wa uhakika umeongeza tija katika shughuli za uzalishaji, umeimarisha mnyororo wa thamani wa mazao ya kilimo kupitia uchakataji, uhifadhi na uongezaji thamani, hatua inayowawezesha wakulima na wajasiriamali kuongeza kipato na ushindani wa bidhaa zao sokoni.
Aidha, amesema maendeleo hayo yameongeza fursa za ajira, kuchochea uwekezaji katika viwanda vidogo na vya kati, kukuza biashara na kuboresha utoaji wa huduma muhimu za kijamii, ili kuimarisha ustawi wa wananchi na uchumi wa vijijini kwa ujumla.
Amesisitiza kuwa REA itaendelea kutekeleza miradi ya kusambaza umeme na kuwaunganisha wananchi na huduma hiyo ili kuhakikisha nishati ya umeme inaendelea kuwa nguzo muhimu ya maendeleo endelevu na utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Aidha, wananchi wanaotembelea banda la REA katika Maonesho ya Nanenane wanaendelea kujifunza kuhusu mafanikio ya utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini na namna huduma hiyo inavyoendelea kufungua fursa za kiuchumi, kuongeza tija katika uzalishaji na kubadilisha maisha ya Watanzania.