Social Links Search User Login Menu
Tools
Close
Close
Vitongoji Vyote 64,359 Vitakuwa na Umeme Ifikapo 2030
Frank A. Mugogo 1226

Vitongoji Vyote 64,359 Vitakuwa na Umeme Ifikapo 2030

Imeelezwa kuwa hadi kufikia mwaka 2030 vitongoji vyote Tanzania Bara vitakuwa vimefikishiwa nishati ya umeme kupitia miradi mbalimbali inayotekelezwa na kusimamiwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Umeme Vijijini kutoka REA, Mhandisi Jones Olotu Julai 05, 2025 katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam ndani ya Banda la Maonesho la Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

"Tayari tumefikisha umeme katika vijiji vyote 12,318 Tanzania Bara sawa na asilimia 100 na sasa hivi ni zamu ya vitongoji, leo hii ninavyozungumza vitongoji 33,657 kati ya vitongoji 64,359 kote nchini vimefikishiwa umeme ambayo ni sawa na asilimia 52.3," alisema Mhandisi Olotu.

Mhandisi Olotu aliweka bayana namna ambavyo Serikali imejizatiti katika kuhakikisha umeme unafika katika kila kona ya nchi kupitia miradi mbalimbali inayotekelezwa kwa usimamizi wa REA ili kuwaletea maendeleo wananchi wake.

Alisema kuwa vitongoji 30,702 havijafikiwa na umeme, hata hivyo alibainisha hatua mbalimbali zilizochukuliwa na zinazoendelea kupitia miradi inayotekelezwa ya kuhakikisha umeme unafika katika vitongoji hivyo.

"Katika vitongoji ambavyo havijafikiwa; vitongoji 7,736 vipo katika miradi inayoendelea kutekelezwa na vitongoji 22,966 kati ya hivi  tumetangaza zabuni kubwa ya kufikisha umeme kwenye vitongoji 9,009 hivyo tutabakiwa na vitongoji 13,957 ambavyo tunatarajia ndani ya miaka mitano navyo vitakuwa vimefikiwa kulingana na upatikanaji wa fedha," alibainisha Mha. Olotu.

Mhandisi Olotu alitoa wito kwa wananchi katika maeneo yaliyofikiwa na umeme kutumia umeme kuboresha hali ya maisha yao kwa kubuni miradi inayotumia umeme ili kujiongezea vipato vyao badala ya kutumia umeme kwa ajili tu ya mwanga wakati wa usiku.

Amewasihi kuiga mfano wa baadhi ya wananchi ambao wamevumbua fursa katika maeneo yao baada ya kufikishiwa umeme jambo ambalo limeanza kuleta manufaa katika maisha yao ya kila siku.

"Baadhi ya wanufaika tumeshuhudia namna ambavyo wamechangamkia uwepo wa umeme kwenye maeneo yao, tumekuta wanatumia umeme kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo saluni, wamefungua kumbi za kuonyesha sinema na mpira, karakana za kuchomelea na wengine wamefungua biashara ya kuuza vinywaji baridi," alisema.

Alisema kuwa katika maeneo mengi ya vijiji miji hali ya maisha imebadilika baada ya kufikishiwa umeme kwani fursa za ajira zimeongezeka kutokana na kuibuliwa kwa viwanda vidogo vidogo vingi vya kuchakata mazao.

Imetolewa na:

Mkurugenzi Mkuu
Wakala wa Nishati Vijijini
Jengo la REA
28 Mtaa wa Medeli
Dodoma

Share

Print
«September 2026»
MonTueWedThuFriSatSun
31123456
789
Rea Yawajengea Uwezo Waendelezaji wa Miradi Midogo ya Umeme Unaozalishwa na Maporomoko ya Maji

Rea Yawajengea Uwezo Waendelezaji wa Miradi Midogo ya Umeme Unaozalishwa na Maporomoko ya Maji

IRINGA, Nyanda za Juu Kusini

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeendelea kuchukua hatua madhubuti katika kuimarisha upatikanaji wa nishati nchini kwa kuendesha mafunzo maalum ya wiki moja yaliyolenga kujenga uwezo wa waendelezaji wa miradi midogo ya uzalishaji wa umeme unaotokana na maporomoko ya maji (Small Hydropower).

Mafunzo hayo yaliyoanza tarehe 7 Septemba, 2026 katika Hoteli ya Sunset mkoani Iringa, yamewakutanisha waendelezaji wa miradi (Developers) zaidi ya 15, hususan kutoka maeneo ya Nyanda za Juu Kusini. Lengo kuu ni kuwajengea uwezo wa kiufundi ili kuongeza ubora wa miradi yao ili iweze kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, tarehe 9 Septemba, 2026, Kaimu Meneja wa Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji Miradi kutoka REA, Mhandisi Emmanuel Yesaya, alisema kuwa REA haishii tu kutoa msaada wa upatikanaji wa nishati vijijini, bali inajikita pia katika kuongeza ujuzi wa wataalamu wa ndani.

"Kuongeza ujuzi kwa waendelezaji hawa kutasaidia kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa kuzingatia viwango vya kitaalamu na ubora unaohitajika. Hatua hii itaongeza idadi ya miradi inayofikia vigezo vya kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa, kuongeza uzalishaji wa umeme, na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii vijijini," alisema Mhandisi Yesaya.

Mafunzo hayo yameendeshwa kwa ushirikiano kati ya REA na Wataalamu kutoka Ndaki ya Uhandisi na Teknolojia (CoET) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM). Maeneo yaliyofundishwa ni pamoja na usanifu wa miradi, upembuzi yakinifu, sayansi ya maji (hydrology), uhandisi wa umeme na elektroniki, pamoja na uendeshaji na matengenezo ya mitambo.

Mbali na mafunzo, REA imebainisha kuwa imekuwa ikisaidia waendelezaji hao kupitia ruzuku za ujenzi, maandalizi ya maandiko ya miradi na usanifu.

Aidha, Wakala huo upo katika mchakato wa kuandaa mfumo wa mikataba ya muda mrefu (Framework Contract) na taasisi za elimu ili kutoa mafunzo endelevu kwenye nishati jadidifu ikiwemo nishati ya jua na mifumo ya gesi vunde.

Kwa upande wao, baadhi ya washiriki wamepongeza mafunzo hayo; akizungumza na Wanahabari, Mhandisi Denis Makoyi kutoka kampuni ya Africa Power Investment, alisema mafunzo hayo yameongeza uelewa mkubwa wa kiufundi katika hatua za utekelezaji wa miradi. Naye Lutengano Kigola kutoka mradi wa Nyalawa Hydropower, aliongeza kuwa mafunzo hayo yanathibitisha kuwa Tanzania ina wataalamu wa ndani wenye uwezo mkubwa wa kuendeleza miradi ya umeme wa maji.

  • MWISHO –

 

Read more
10111213
14
REA Yaendelea Kuwezesha Miradi ya Umeme wa Maji Nyanda za Juu Kusini

REA Yaendelea Kuwezesha Miradi ya Umeme wa Maji Nyanda za Juu Kusini

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeendelea kuwezesha waendelezaji wadogo wa miradi ya uzalishaji wa umeme unaotokana na maporomoko ya maji (Small Hydropower) katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kwa kutoa fedha, msaada wa kitaalamu na mafunzo, hatua inayolenga kuongeza uzalishaji wa nishati nchini.

Read more
151617181920
21222324252627
2829301234
567891011

Archive

Contact Us

E-Mail
General Information:  info@rea.go.tz
Director General:  dg@rea.go.tz
Procurement (PMU):  pmu@rea.go.tz
Webmaster:  webmaster@rea.go.tz

Mailing Address

Director General
Rural Energy Agency - REA
REA Building
28 Medeli Street
P. O. Box 2153
Dodoma, Tanzania

Phone & Fax

Tel: +255 26 2323504, +255 26 2323506
+255 26 2323507
Fax: +255 26 2323507

Time Zone

Please note that we are based in Tanzania, Time zone (GMT+03:00). Although we may not be in office at times convenient for all international enquiries, we do monitor our e-mail outside normal office hours.

Back To Top