WATEJA 22,700 KUNUFAIKA NA MRADI WA UMEME KUTOKA MAKAMBAKO HADI SONGEA
WATEJA 22,700 KUNUFAIKA NA MRADI WA KUSAMBAZA UMEME KATIKA VIJIJI VINAVYOPITIWA NA MKUZA WA MRADI WA UMEME KUTOKA MAKAMBAKO HADI SONGEA
Jumla ya wateja wa awali 22,700 wanatarajiwa kuunganishiwa na huduma ya umeme kupitia Mradi wa Kusambaza Umeme katika mkuza wa njia kuu ya kusafirisha umeme wa kilovolti 220 kutoka Makambako hadi Songea. Mradi huu unatekelezwa katika mikoa ya Ruvuma na Njombe ambapo jumla ya vijiji 122 vinatarajiwa kupelekewa miundombinu ya kusambaza umeme na tayari vijiji 110 vimefikishiwa huduma ya umeme.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mradi huo tarehe 06/04/2019, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli aliwataka wananchi wanaoishi katika vijiji vilivyopo katika mradi huo kutumia umeme kwa ajili ya shughuli za uzalishaji mali kwa kuanzisha viwanda vidogo vidogo na kuleta maendeleo. Aidha, Rais aliagiza vijiji vyote ambavyo havina umeme visambaziwe miundombinu na kuwezesha upatikanaji wa huduma ya umeme katika vijiji hivyo.
Awali Bodi ya Nishati Vijijini (REB) iliwahakikishia wananchi waishio maeneo ya vijijini nchini kuwa watapelekewa huduma ya umeme kupitia Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili ambao utakamilisha ujenzi wa miundombinu ya umeme katika vijiji vyote ambavyo bado havijafikiwa na miundombinu ya umeme.
Naye Balozi wa Sweden nchini Tanzania, Anders Sjöberg ambaye nchi yake imefadhili mradi huo alisema anaamini kuwa kukamilika kwa mradi huo kutaimarisha utoaji wa huduma za afya, elimu, maji pamoja na kuongeza kipato hivyo kupunguza umaskini.
Mkurugenzi Mkuu
Wakala wa Nishati Vijijini (REA)
Mawasiliano Towers, Ghorofa ya 2
Barabara ya Sam Nujoma
S. L. P 7990
Dar es Salaam, Tanzania
Barua Pepe: info@rea.go.tz
Simu: +255 22 2412001, +255 22 2412002, +255 22 2412003
Nukushi: +255 22 2412007