BALOZI WA NORWAY ATEMBELEA OFISI ZA WAKALA WA NISHATI VIJIJINI (REA)
Balozi wa Norway nchini Tanzania, Ms. Elisabeth Jacobsen ametembelea Ofisi za Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na kufanya mazungumzo na Menejimenti ya Wakala tarehe 28 Februari, 2019.
Katika mazungumzo hayo, Mh. Balozi alisema ziara yake hiyo ina lengo la kuimarisha ushirikiano kati ya Wakala na Ubalozi ikizingatiwa kuwa sekta ya nishati ni moja ya maeneo ya kipaumbele kwa nchi ya Norway katika ushirikiano. Aliongeza kuwa, sekta ya nishati imevutia wawekezaji na imesaidia kukuza sekta binafsi.
Awali Balozi Jacobsen na ujumbe wake walitembelea wajasiriamali katika Wilaya ya Mkuranga ambao wamenufaika na miradi ya kusambaza umeme vijijini. Mh. Balozi alisema wamevutiwa na shughuli za uzalishaji mali ambazo zimeibuka katika maeneo ya vijijiini kutokana na upatikanaji wa huduma za umeme hivyo kuwawezesha wananchi kuongeza kipato na kubadilisha hali za maisha yao.
Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini ilishukuru na kusisitiza ushirikiano wa wadau katika utekelezaji wa miradi ya kusambaza nishati vijijini ili kuweza kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Awali akiwakaribisha wageni hao, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mha. Amos Maganga aliishukuru Serikali ya Norway kwa kufadhili miradi ya kusambaza umeme vijijini na kuwaomba waendelee kutoa ufadhili kwa Serikali ili iweze kusambaza nishati katika maeneo ya visiwa zaidi ya 100 vilivyopo katika maziwa mbalimbali na Bahari ya Hindi.
Mkurugenzi Mkuu
Wakala wa Nishati Vijijini (REA)
Mawasiliano Towers, Ghorofa ya 2
Barabara ya Sam Nujoma
S. L. P 7990
Dar es Salaam, Tanzania
Barua Pepe: info@rea.go.tz
Simu: +255 22 2412001, +255 22 2412002, +255 22 2412003
Nukushi: +255 22 2412007