Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kushirikiana na kampuni ya Oryx Gas Tanzania, tarehe 12 Februari, 2025 imeanza rasmi kusambaza mitungi ya gesi ya kilo 6 kwa wakazi wa mkoa wa Songwe na kwa kuanzia Wananchi wa wilaya ya Mbozi wameanza kununua mitungi hiyo kwa nusu bei.
Mkuu wa mkoa wa Songwe, Mhe. Daniel Chongolo amewapongeza REA pamoja na msambazaji, kampuni ya Oryx Gas kwa kuanza kugawa mitungi hiyo katika muda muhafaka na kutoa wito kwa REA na wasambazaji kuendelea kutoa elimu kuhusu usalama wa gesi; na faida ya matumizi ya nishati safi na salama kiafya na namna zinvyochangia katika utunzaji na uhifadhi mazingira.
“Mpango huu wa kusambaza mitungi ya gesi ni mzuri na kama mnavyofahamu; Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Mama Samia Suluhu Hassan ni Mhamasishaji namba moja wa nishati safi siyo tu barani Afrika bali Duniani kote, kwa ujumla na sisi tunaoishi mikoa ya pembezoni, ndiyo waathirika wakubwa wa changamoto zinazotokana na matumizi ya nishati zisizo safi.”
"Naipongeza REA kwa kuanza kutekeleza Mradi huu, nawapongeza pia Oryx Gas kwa kuwa sehemu ya ajenda ya kusambaza nishati safi kwa Watanzani. Huu ni uzalendo wa hali ya juu kwa Taifa letu” amesema Mhe. Chongolo.
Kwa upande wake, Meneja Mradi wa Nishati Safi mkoa wa Songwe kutoka REA; Bwana Vencha Maganga amesema, Serikali kupitia REA imetenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa Miradi ya kusambaza nishati safi ikiwemo gesi (LPG) katika maeneo ya vijijini na pembezoni mwa miji na kuwaomba Wananchi wa mkoa wa Songwe kuchangamkia fursa ya kununua mitungi ya gesi kwa bei ya ruzuku ambayo ni shilingi 20,000 tu kwa mtungi wa gesi wa kilo sita (6) na fedha inayobaki, inalipwa na Serikali.
"Lengo letu ni kutoa elimu na kuwawezesha Wamama ambao ndiyo watumiaji wakubwa wa nishati chafu ili wapate nishati safi ya kupikia kwa ajili ya kupunguza athari zinazotokana na matumizi ya nishati zisizo safi. Nawaomba Wananch wafike kwenye vituo vya kuuzia mitungi hiyo, wakiwa na Vitambulisho vya NIDA kwa ajili kununua mitungi hii pamoja na vifaa vyake kwa bei ya ruzuku ya shilingi (20,000/=) tofauti na ambavyo wangenunua kwa shilingi (40,000) na kuendelea hadi shilingi (60,000)”. Ameongeza Bwana Maganga.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mbozi; Mhe. George Msyani amewapongeza Wananchi kufika kwenye kituo cha mauzo ili kununua mitungi hiyo ya gesi kwa bei ya ruzuku katika kitongoji cha Mlowo, wilayani Mbozi.
Wilaya zitakazonufaika na usambazaji wa mitungi hiyo ya gesi kwa mkoa wa Songwe ni pamoja Mbozi, Ileje, Momba na Songwe
Imetolewa na:
Mkurugenzi Mkuu
Wakala wa Nishati Vijijini
Jengo la REA
28 Mtaa wa Medeli
Dodoma