UZINDUZI WA MRADI WA UMEME VIJIJINI AWAMU YA TATU MKOA WA SINGIDA
Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umezindua utekelezaji wa Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu katika Mkoa wa Singida. Mgeni rasmi Katika uzinduzi huo uliofanyika tarehe 24/03/2017 katika kijiji cha Mkwese Wilaya ya Manyoni alikuwa ni Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo.
Mradi huu unajumuisha vipengele-mradi vitatu vya Grid Extension, Densification ambayo inalenga kuongeza wigo wa usambazaji umeme kwenye vijiji ambavyo vimefikiwa na miundombinu ya umeme lakini baadhi ya vijiji na vitongoji havikuungwa. Kipengele-mradi cha tatu kinahusisha usambazaji wa nishati jadidifu kwenye maeneo yaliyo mbali na gridi.
Utekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu katika Mkoa wa Singida utahusisha vipengele vyote vitatu. Mradi huu utatekelezwa kwa vipindi viwili tofauti. Sehemu ya awali itahusisha upelekaji umeme katika vijiji 185 kwa gharama ya Shilingi Bilioni 47.36. Utekelezaji wa sehemu hii ya kwanza umeanza Mwezi Februari 2017 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Machi 2019.
Aidha, sehemu ya pili ya mradi huu wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu itaanza kutekelezwa baada ya sehemu ya kwanza kukamilika Mwaka 2019 ambapo vijiji 82 vitapatiwa umeme na hivyo kufikisha umeme katika vijiji vyote vya mkoa wa Singida ifikapo Mwaka 2021.
Imetolewa na:
Mkurugenzi Mkuu
Wakala wa Nishati Vijijini (REA)
Mawasiliano Towers, Ghorofa ya 2
Barabara ya Sam Nujoma
S. L. P 7990
Dar es Salaam, Tanzania
Barua Pepe: info@rea.go.tz
Simu: +255 22 2412001, +255 22 2412002, +255 22 2412003
Nukushi: +255 22 2412007