Social Links Search User Login Menu
Tools
Close
Close
Wakandarasi wa REA Wahimizwa Kuunganishia Wateja Umeme kwa Kutumia UMETA
Admin.Frank Mugogo 8524

Wakandarasi wa REA Wahimizwa Kuunganishia Wateja Umeme kwa Kutumia UMETA

Wakandarasi wanaotekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya III Mzunguko wa I wameagizwa kuwaunganisha wananchi walio katika eneo la mradi kwa kutumia kifaa cha Umeme Tayari (UMETA) ambacho ni mbadala wa kufunga mfumo wa nyaya katika nyumba (wiring) ili kuepuka kuruka nyumba zilizofikiwa na miundombinu ya umeme.

Agizo hilo lilitolewa tarehe 23 Oktoba 2019 na Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi ya Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhandisi Styden Rwebangira katika kikao cha majumuisho ambacho kilihudhuriwa na Wajumbe wa Kamati ya Ufundi ya Bodi ya Nishati Vijijini, Menejimenti ya Wakala wa Nishati Vijijini, Wakandarasi na Mameneja wa TANESCO wa wilaya zote za Mkoa wa Tanga baada ya ukaguzi wa utekelezaji wa mradi huo katika Mkoa wa Tanga ambapo aliwataka wakandarasi wahakikishe wanagawa UMETA 250 za bure ambazo zimetolewa na Serikali kwa wananchi wote ambao hawajafunga mfumo wa nyaya katika nyumba zao.

Mhandisi Rwebangira alisema kwa ujumla wameridhishwa na kazi ya utekelezaji wa mradi huo katika Mkoa wa Tanga. “Tunaridhishwa na utendaji wa wakandarasi, changamoto ni kwamba vifaa vya UMETA havifungwi kwenye nyumba za wananchi” aliongeza.

Aidha alisema kuwa changamoto nyingine ambayo wameibaini ni uhaba wa nyaya zinazotumika katika ujenzi wa miundombinu ya kusambazia umeme na kuwa suala hilo linafuatiliwa na Bodi ya NIshati Vijijini pamoja na Waziri wa Nishati ambapo kutakuwa na kikao cha watengenezaji wa nyaya tarehe 29 oktoba 2019 ili kuweka mkakati wa upatikanaji wa nyaya na kuwawezesha wakandarasi kukamilisha mradi kwa wakati.

Mhandisi Rwebangira aliwahimiza wakandarasi wote wanaotekeleza mradi huo nchini kukamilisha kazi ifikapo tarehe 31 Desemba 2019 ili kutoa nafasi kwa mzunguko wa pili wa mradi huo kuanza Mwezi Januari 2020 bila ya viporo vya kazi za mzunguko wa kwanza. Aliwatahadharisha wakandarasi ambao hawatakamilisha kazi wanaweza wakakosa fursa ya kuomba tena kazi za kusambaza umeme katika mzunguko wa pili zitakapotangazwa.

Akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Jones Olotu aliwahimiza wakandarasi kuhakikisha kuwa wamepeleka vifaa vyote katika maeneo ya mradi kabla msimu wa mvua haujaanza ili kuepuka usumbufu wa kusafirisha vifaa hivyo kipindi cha mvua.

Wakandarasi walisema wamepokea agizo la kukamilisha mradi ifikapo 31 Desemba 2019 na kuiomba REB ihakikishe kuwa nyaya zinazotumika katika ujenzi wa miundombinu ya kusambazia umeme zinapatikana kutoka kwa wazalishaji wa ndani kwa wakati. Msimamizi wa Mradi wa Kampuni ya Derm Electric, Mhandisi Aziz Msuya alisema kuwa utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 83.5 na kuwa nguzo zimesimikwa katika vijiji 24 na kimebaki kijiji kimoja tu kusimikwa nguzo hadi kufikia tarehe hiyo. Alisema changamoto ni jiografia ambayo inasumbua kusafirisha nguzo katika maeneo ya milimani.

Naye Mkurugenzi wa Kampuni ya Njarita, Michael Njarita alisema kuwa wamefikia asilimia 67.8 ya utekelezaji wa mradi na kuwa changamoto kubwa ni upatikanaji wa nyaya na mabadiliko ya hali ya hewa. “Lengo la kumaliza mradi ifikapo tarehe 31 Desemba 2019 lipo palepale, tutajitahidi kumaliza kwa wakati” alisema.

Akizungumzia manufaa ya mradi huo, Katibu Tawala Msaidizi wa Mkoa wa Tanga, Bw. Sebastian Masanja alisema upatikanaji wa huduma ya umeme vijijini unachochea ukuaji wa uchumi kwa kuongeza ajira katika sekta isiyo rasmi na kutoa fursa kwa vijana wengi kujiari kwa kuanzisha biashara za kuchomelea vyuma, gereji, maduka, salon za kunyolea nywele na mabanda ya kuonesha mipira.


Mkurugenzi Mkuu
Wakala wa Nishati Vijijini (REA)
Jengo la LAPF, Ghorofa ya 7
S. L. P 2153
Dodoma, Tanzania

Barua pepe: info@rea.go.tz
Simu: +255 262323504, +255 262323506, +255 262323507

Share

Print
«September 2026»
MonTueWedThuFriSatSun
31123456
789
Rea Yawajengea Uwezo Waendelezaji wa Miradi Midogo ya Umeme Unaozalishwa na Maporomoko ya Maji

Rea Yawajengea Uwezo Waendelezaji wa Miradi Midogo ya Umeme Unaozalishwa na Maporomoko ya Maji

IRINGA, Nyanda za Juu Kusini

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeendelea kuchukua hatua madhubuti katika kuimarisha upatikanaji wa nishati nchini kwa kuendesha mafunzo maalum ya wiki moja yaliyolenga kujenga uwezo wa waendelezaji wa miradi midogo ya uzalishaji wa umeme unaotokana na maporomoko ya maji (Small Hydropower).

Mafunzo hayo yaliyoanza tarehe 7 Septemba, 2026 katika Hoteli ya Sunset mkoani Iringa, yamewakutanisha waendelezaji wa miradi (Developers) zaidi ya 15, hususan kutoka maeneo ya Nyanda za Juu Kusini. Lengo kuu ni kuwajengea uwezo wa kiufundi ili kuongeza ubora wa miradi yao ili iweze kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, tarehe 9 Septemba, 2026, Kaimu Meneja wa Usaidizi wa Kiufundi kwa Waendelezaji Miradi kutoka REA, Mhandisi Emmanuel Yesaya, alisema kuwa REA haishii tu kutoa msaada wa upatikanaji wa nishati vijijini, bali inajikita pia katika kuongeza ujuzi wa wataalamu wa ndani.

"Kuongeza ujuzi kwa waendelezaji hawa kutasaidia kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa kuzingatia viwango vya kitaalamu na ubora unaohitajika. Hatua hii itaongeza idadi ya miradi inayofikia vigezo vya kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa, kuongeza uzalishaji wa umeme, na kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii vijijini," alisema Mhandisi Yesaya.

Mafunzo hayo yameendeshwa kwa ushirikiano kati ya REA na Wataalamu kutoka Ndaki ya Uhandisi na Teknolojia (CoET) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM). Maeneo yaliyofundishwa ni pamoja na usanifu wa miradi, upembuzi yakinifu, sayansi ya maji (hydrology), uhandisi wa umeme na elektroniki, pamoja na uendeshaji na matengenezo ya mitambo.

Mbali na mafunzo, REA imebainisha kuwa imekuwa ikisaidia waendelezaji hao kupitia ruzuku za ujenzi, maandalizi ya maandiko ya miradi na usanifu.

Aidha, Wakala huo upo katika mchakato wa kuandaa mfumo wa mikataba ya muda mrefu (Framework Contract) na taasisi za elimu ili kutoa mafunzo endelevu kwenye nishati jadidifu ikiwemo nishati ya jua na mifumo ya gesi vunde.

Kwa upande wao, baadhi ya washiriki wamepongeza mafunzo hayo; akizungumza na Wanahabari, Mhandisi Denis Makoyi kutoka kampuni ya Africa Power Investment, alisema mafunzo hayo yameongeza uelewa mkubwa wa kiufundi katika hatua za utekelezaji wa miradi. Naye Lutengano Kigola kutoka mradi wa Nyalawa Hydropower, aliongeza kuwa mafunzo hayo yanathibitisha kuwa Tanzania ina wataalamu wa ndani wenye uwezo mkubwa wa kuendeleza miradi ya umeme wa maji.

  • MWISHO –

 

Read more
10111213
14
REA Yaendelea Kuwezesha Miradi ya Umeme wa Maji Nyanda za Juu Kusini

REA Yaendelea Kuwezesha Miradi ya Umeme wa Maji Nyanda za Juu Kusini

Wakala wa Nishati Vijijini (REA) umeendelea kuwezesha waendelezaji wadogo wa miradi ya uzalishaji wa umeme unaotokana na maporomoko ya maji (Small Hydropower) katika mikoa ya Nyanda za Juu Kusini kwa kutoa fedha, msaada wa kitaalamu na mafunzo, hatua inayolenga kuongeza uzalishaji wa nishati nchini.

Read more
151617181920
21222324252627
2829301234
567891011

Archive

Contact Us

E-Mail
General Information:  info@rea.go.tz
Director General:  dg@rea.go.tz
Procurement (PMU):  pmu@rea.go.tz
Webmaster:  webmaster@rea.go.tz

Mailing Address

Director General
Rural Energy Agency - REA
REA Building
28 Medeli Street
P. O. Box 2153
Dodoma, Tanzania

Phone & Fax

Tel: +255 26 2323504, +255 26 2323506
+255 26 2323507
Fax: +255 26 2323507

Time Zone

Please note that we are based in Tanzania, Time zone (GMT+03:00). Although we may not be in office at times convenient for all international enquiries, we do monitor our e-mail outside normal office hours.

Back To Top