Social Links Search User Login Menu
Tools
Close
Close
MPANGO KABAMBE UPELEKAJI NISHATI VIJIJINI WABAINISHWA
Admin.Frank Mugogo 906

MPANGO KABAMBE UPELEKAJI NISHATI VIJIJINI WABAINISHWA

Na Veronica Simba - Kigoma

Imeelezwa kuwa Mpango Kabambe wa Kupeleka Nishati Vijijini umelenga kuwanufaisha wananchi kupitia usambazaji umeme pamoja na nishati bora ya kupikia.

Hayo yalibainishwa mwishoni mwa wiki wakati wa ziara ya viongozi wakuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) mkoani Kigoma.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB) Wakili Julius Kalolo na Mkurugenzi Mkuu wa REA Mhandisi Hassan Saidy, walisema kuwa Mpango huo unahusisha nishati za aina mbalimbali, siyo umeme peke yake.

Wakili Kalolo alisema kuwa, ni jukumu la REA kuhakikisha wananchi waishio vijijini wanapata nishati safi na zenye gharama nafuu ili ziwasaidie kuboresha maisha yao, hivyo Wakala umejiwekea mikakati ya kuhakikisha jukumu hilo linatekelezwa ipasavyo.

Akifafanua, alisema kuwa REA imefanikiwa kwa kiasi kikubwa na inaendelea kufanya vema katika utekelezaji wa miradi ya umeme vijijini, hivyo hakuna shaka katika utekelezaji wa miradi ya aina nyingine za nishati zilizofanyiwa tafiti, utakuwa wenye ufanisi pia.

Akitoa mfano, alisema kuwa tafiti zinaonesha eneo jingine muhimu linalopaswa kupewa kipaumbele ni katika nishati ya kupikia ambapo asilimia kubwa ya waathirika ni wanawake, ambao kutokana na matumizi ya kuni, wamekuwa wakisumbuliwa na magonjwa ya macho na kifua.

Alisema, ni kwa sababu hiyo, Wakala umedhamiria kuondoa adha hiyo katika jamii hususani wanawake waishio vijijini.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu akidadavua zaidi kuhusu Mpango huo kabambe, alieleza kuwa umejikita katika sehemu mbili kubwa ambazo ni usambazaji umeme pamoja na nishati ya kupikia.

Alieleza zaidi kuwa, hivi sasa, Wakala unaongeza nguvu zaidi katika nishati ya kupikia ili kuhakikisha kwamba wananchi hususan wa vijijini, wanatumia nishati bora kwa shughuli za kupikia na kupunguza au kuachana kabisa na matumizi ya kuni na mkaa ambao upatikanaji wake ni mgumu, aghali na siyo rafiki kwa mazingira.

Mhandisi Saidy alisema REA imefanya tafiti kadhaa za majaribio kuhusu nishati ya kupikia mathalani mradi wa kutumia tungamotaka, ambapo mifumo husika ilipelekwa katika maeneo 725 yaliyopo sehemu mbalimbali nchini.

Aidha, aliongeza kuwa, Wakala umeshirikiana na kampuni za usambazaji gesi kufanya tafiti kuhusu uwezekano wa kuhakikisha nishati ya gesi inafikishwa katika maeneo ya vijijini kwa gharama nafuu ili wananchi waweze kuitumia kwa shughuli za kupikia.

Katika hatua nyingine, viongozi hao waliwahakikishia Wakuu wa Wilaya za Kibondo na Kakonko, ambao walikutana nao kwa nyakati tofauti, kuwa maeneo yote ya kimkakati, hasa yanayohusisha masuala ya usalama yatapelekewa huduma ya umeme ili kuwezesha shughuli hizo kufanyika kwa ufanisi.

Awali, Mkuu wa Wilaya ya Kakonko Kanali Evance Malassa na Mkuu wa Wilaya ya Kibondo Kanali Aggrey Magwaza, kwa nyakati tofauti waliomba maeneo ya mpakani ambayo hayajafikiwa na huduma ya umeme, yapewe kipaumbele katika kufikishiwa nishati hiyo ili kuimarisha shughuli za kiusalama.

Pia, Wakuu hao wa Wilaya walipongeza jitihada ambazo zimekuwa zikifanywa na Wakala wa Nishati Vijijini katika kusambaza umeme vijijini kupitia miradi mbalimbali inayoendelea kutekelezwa.

Katika ziara hiyo, Mwenyekiti wa Bodi na Mkurugenzi Mkuu pia walikagua miradi mbalimbali ya umeme pamoja na kukutana na wakandarasi wanaotekeleza miradi hiyo ambapo walijadili changamoto zilizopo na kuzipatia ufumbuzi.

Kupitia kikao hicho, viongozi hao waliipatia ufumbuzi changamoto ya upatikanaji vifaa iliyokuwa ikimkabili Mkandarasi anayetekeleza Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Kwanza, Kampuni Tanzu ya TANESCO (ETDCO) katika wilaya za Kakonko na Kibondo.

“Utekelezaji ulikuwa nyuma kidogo kutokana na changamoto ya vifaa. Tumetatua changamoto hiyo na tumemwelekeza Mkandarasi ndani ya miezi mitatu awe amekamilisha mradi huu,” alisema Mkurugenzi Mkuu.

Aidha, Mkandarasi anayetekeleza Mradi huo katika wilaya za Buhigwe, Kasulu, Kigoma Vijijini na Uvinza, Kampuni ya M/s CCCE Etern Consortium alielekezwa kuongeza nguvu ili akamilishe kazi hiyo kwa wakati uliopangwa ambao ni mwishoni mwa mwezi huu wa Desemba, 2021.

Miradi mingine inayotekelezwa mkoani Kigoma ni pamoja na REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili unaotarajiwa kuanza hivi karibuni pamoja na Mradi wa Ujazilizi unaolenga kufikisha umeme katika maeneo yaliyopitiwa na miundombinu ya nishati hiyo lakini umeme haujashushwa.

Katika ziara hiyo, viongozi hao wa REA waliambatana na wataalamu mbalimbali kutoka Wakala hiyo pamoja na Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).

Mkurugenzi Mkuu
Wakala wa Nishati Vijijini (REA)
Jengo la PSSSF, Ghorofa ya 7
Barabara ya Makole
S. L. P 2153
Dodoma, Tanzania
Barua pepe: info@rea.go.tz

Simu: +255 262323504, +255 262323506, +255 262323507

Rate article

No rating
Rate this article:
No rating

Share

Print
«March 2024»
MonTueWedThuFriSatSun
26272829123
45678910
11121314151617
18192021222324
25
Mkopo Nafuu wa Uwezeshaji wa  Ujenzi na Uendeshaji wa Vituo Vidogo vya Bidhaa za  Mafuta (Petroli na Dizeli) Vijijini

Mkopo Nafuu wa Uwezeshaji wa Ujenzi na Uendeshaji wa Vituo Vidogo vya Bidhaa za Mafuta (Petroli na Dizeli) Vijijini

Wakala wa Nishati Vijijini unakaribisha maombi ya mkopo nafuu kuwezesha ujenzi wa vituo vidogo vya kuuzia bidhaa za mafuta (petroli na dizeli) vijijini. Mkopo huu utasaidia uwezeshaji wa ujenzi na uendeshaji wa vituo vipya vidogo vya gharama nafuu maeneo ya vijijini ili kuhakikisha upatikanaji wa nishati ya mafuta kwa gharama nafuu, kwa njia salama, na isiyo na madhara kwa mazingira.

Wakala unawasisitiza waombaji walioomba katika awamu ya kwanza na kutokidhi vigezo kuomba tena baada ya kufanya marekebisho  ya  mapungufu yaliyobainishwa katika maombi yao. Aidha maombi mapya ya mkopo yanakaribishwa.

Read more
262728293031
1234567

Archive

Contact Us

E-Mail
General Information:  info@rea.go.tz
Director General:  dg@rea.go.tz
Procurement (PMU):  pmu@rea.go.tz
Webmaster:  webmaster@rea.go.tz

Mailing Address

Director General
Rural Energy Agency - REA
PSSSF Building, 7th Floor
Makole Road
P. O. Box 2153
Dodoma, Tanzania

Phone & Fax

Tel: +255 26 2323504, +255 26 2323506
+255 26 2323507
Fax: +255 26 2323507

Time Zone

Please note that we are based in Tanzania, Time zone (GMT+03:00). Although we may not be in office at times convenient for all international enquiries, we do monitor our e-mail outside normal office hours.

Back To Top